HAYA NI YA TFF YA LEO




LYON KUJUA MUSTAKABALI WAKE CHAMAZI
HATMA ya African Lyon kuendelea kushika mkia au la kwenye Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inajulikana kesho wakati itakapokuwa mwenyeji wa Ruvu Shooting kwenye Uwanja Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam.

Lyon yenye pointi 13 kutokana na mechi 19 inabidi iifunge Ruvu Shooting kama inataka kuirejesha mkiani Toto African yenye pointi 14. Kama kweli inazitaka pointi zote tatu itabidi ifanye kazi mbele ya Ruvu Shooting inayotiwa makali na Kocha Charles Boniface Mkwasa.

Hiyo itakuwa mechi ya 18 kwa Ruvu Shooting inayoshika nafasi ya saba ikiwa na pointi 26 ikitanguliwa na vinara wa ligi hiyo Yanga, Azam, Simba, Coastal Union, Kagera Sugar na Mtibwa Sugar yenye pointi 28 ikinolewa na nahodha wa zamani wa Taifa Stars, Mecky Maxime.

Mechi hiyo namba 139 itachezeshwa na mwamuzi Amon Paul kutoka Musoma wakati wasaidizi ni Anold Bugado wa Singida na Milambo Tshikungu kutoka Mbeya. Mwamuzi wa mezani atakuwa Shafii Mohamed wa Dar es Salaam.

Nayo Tanzania Prisons ya Jumanne Chale itakuwa mgeni wa Oljoro JKT katika mechi itakayochezwa Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha wakati Mgambo Shooting itaoneshana kazi na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

Keshokutwa (Machi 7 mwaka huu) Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya JKT Ruvu ya Kocha Charles Kilinda na Kagera Sugar.

Ligi hiyo itaendelea tena Jumamosi ya Machi 9 mwaka huu kwa mechi mbili; Yanga vs Toto Africans (Uwanja wa Taifa), na Azam vs Polisi Morogoro (Azam Complex, Chamazi).


TFF YAWASILISHA RASMI MAOMBI KUMUONA WAZIRI
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limewasilisha rasmi maombi ya kuonana na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara ili kuzungumzia uamuzi wake wa kutengua usajili wa Katiba ya 2012.

Maombi hayo yaliwasilishwa rasmi Wizarani jana (Machi 4 mwaka huu) ambapo TFF imependekeza kikao hicho kifanyike keshokutwa (Machi 7 mwaka huu) au Machi 13 mwaka huu.

Kamati ya Utendaji ya TFF iliyokutana Machi 2 mwaka huu kujadili tamko ya Waziri kutengua matumizi ya Katiba ya 2012 ndiyo iliyopendekeza kikao hicho kwa lengo la kusikiliza upande wa TFF katika suala hilo.

HAYA NI YA TFF HII LEO.

FIFA YAWASILISHA MAREKEBISHO 10 YA KATIBA KWA WARAKA
Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limetuma mapendekezo 10 ya marekebisho ya Katiba yake kwa wanachama wake kwa njia ya waraka.

Mapendekezo hayo yametumwa kwa kila nchi mwanachama kupitia waraka namba 1320, ambapo wanachama kwa kupitia kwa mashirikisho yao ya mabara watapiga kura ya ndiyo au hapa. Kwa upande wa Afrika, wanachama wa FIFA wanatakiwa kuwasilisha kura zao kupitia Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).

Baadhi ya mapendekezo hayo ni wajumbe wa Kamati ya Utendaji kuthibitishwa na Mkutano Mkuu wa FIFA (FIFA Congress). Makamu wa Rais wa FIFA na wajumbe wa Kamati ya Utendaji wanaochaguliwa katika mabara ambapo itabidi wathibitishwe na FIFA Congress.

Muundo wa Kamati ya Utendaji; nafasi moja ya vyama vya mpira wa miguu vya Uingereza (British FAs) sasa inahamishiwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Ulaya (UEFA). Pia Mwenyekiti wa Kamati ya Ukaguzi ya FIFA anatakiwa kushiriki vikao vya Kamati ya Utendaji bila kuwa na haki ya kupiga kura.

Uchaguzi wa Rais; mgombea anatakiwa kuungwa mkono na idadi ya kutosha ya vyama wanachama kutoka katika mabara mawili tofauti. Ukomo wa uongozi; kuanzisha vipindi vya uongozi. Ukomo wa umri; ukomo wa umri usiozidi miaka 72 wakati wa kugombea utekelezwe.

Uwakilishi wa kutosha kwa makundi yenye maslahi katika FIFA; makundi yenye maslahi katika mpira wa miguu kama wachezaji wapate uwakilishi katika Kamati ya Mpira wa Miguu. Uteuzi wa mwenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia; uteuzi sasa ufanywe na Mkutano Mkuu wa TFF.

WATAZAMAJI 13,398 WAZISHUHUDIA YANGA, KAGERA
Watazamaji 13,398 wameshuhudia pambano la Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya Yanga na Kagera Sugar lililochezwa juzi (Februari 27 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kuingiza sh. 77,117,000.

Mechi hiyo namba 130 iliyochezeshwa na Simon Mberwa kutoka mkoani Pwani ilimalizika kwa Yanga ambao wanaongoza VPL wakiwa na pointi 42 kuibuka na ushindi wa bao 1-0 lililofungwa dakika ya 45 na Haruna Niyonzima.

Viingilio vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 18,291,297.95 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 11,763,610.17.

Kiingilio cha sh. 5,000 ndicho kilichovutia watazamaji wengi ambapo waliokata tiketi hizo walikuwa 11,908 na kuingiza sh. 59,540,000 wakati idadi ndogo ya washabiki ilikuwa ya kiingilio cha sh. 20,000 kilichovutia washabiki 80 na kuingiza sh. 1,600,000.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 9,300,659.97, tiketi sh. 3,348,990, gharama za mechi sh. 5,580,395.98, Kamati ya Ligi sh. 5,580,395.98, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 2,790,197.99 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 2,170,153.99.

POLISI KUIKABILI OLJORO KUNG’ANG’ANIA VPL
Polisi Morogoro inaikaribisha Oljoro JKT ya Arusha kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro katika mechi pekee ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara itakayochezwa kesho (Machi 2 mwaka huu).

Hata hivyo, timu hizo haziko katika kinyang’anyiro cha kuwania ubingwa ambapo Yanga ndiyo inayoongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 42 wakati Oljoro JKT inayofunzwa na Alex Mwamgaya ikiwa nazo 21 na Polisi Morogoro pointi 15.

Oljoro JKT iko katika nafasi ya tisa. Polisi Morogoro ambayo katika mzunguko wa pili imebadilika ikiwa chini ya Kocha Adolf Rishard inashika nafasi ya 12 ikiziacha mkiani Toto Africans yenye pointi 14 na African Lyon ambayo ina pointi 13.

Ligi hiyo itaendelea Jumatano (Machi 6 mwaka huu) kwa mechi kati ya Oljoro JKT vs Tanzania Prisons (Sheikh Kaluta Amri Abeid), African Lyon vs Ruvu Shooting (Azam Complex, Chamazi) na Mgambo Shooting vs Mtibwa Sugar (Mkwakwani) wakati Machi 7 mwaka huu ni JKT Ruvu vs Kagera Sugar (Azam Complex, Chamazi).

Machi 9 mwaka huu kutakuwa na mechi mbili; Yanga vs Toto Africans 9Uwanja wa Taifa), na Azam vs Polisi Morogoro (Azam Complex, Chamazi).

VILLA SQUAD KUIVAA ASHANTI UNITED FDL
Michuano ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inaendelea kesho (Machi 2 mwaka huu) katika makundi yote matatu. Villa Squad itaivaa Ashanti United kwenye Uwanja wa Karume, Dar es Salaam katika moja ya mechi za kundi B.

Kundi A ni mechi kati ya Kurugenzi ya Mafinga dhidi ya Mbeya City wakati Polisi Iringa vs JKT Mlale, na Majimaji vs Mkamba Rangers zilizokuwa zicheze kesho (Machi 2 mwaka huu), sasa zitaumana Machi 3 mwaka huu mjini Iringa na mjini Songea.

Pia kundi B kesho (Machi 2 mwaka huu) ni Green Warriors vs Transit Camp (Mlandizi) wakati keshokutwa (Machi 3 mwaka huu) Polisi Dar vs Tessema (Karume) na Ndanda vs Moro United katika Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara.

Mechi za kundi C kesho ni JKT Kanembwa vs Polisi Tabora (Lake Tanganyika), Polisi Mara vs Polisi Dodoma (Karume, Musoma), Morani vs Pamba (Kiteto) na Mwadui vs Rhino Rangers (Kambarage, Shinyanga).

SIMBA KUONDOKA NCHINI KESHO

KIKOSI kamili cha Simba kinaondoka jijini Dar es Salaam kesho kikiwa na msafara wa watu 18, wakiwamo wachezaji 18 na viongozi saba.
 
Wachezaji wanaoondoka ni Juma Kaseja, Abel Dhaira, Nassor Said Masoud, Amir Maftah, Koman Bili Keita, Juma Nyoso, Shomari Kapombe, Salim Kinje, Ramadhani Chomboh, Amri Kiemba, Haruna Moshi, Kiggi Makasi, Abdallah Seseme, Amri Kiemba, Haruni Chanongo, Mrisho Ngassa, Felix Sunzu na Abdallah Juma.
 
Viongozi ni Zacharia Hans Poppe, Muhsin Balhabou, Patrick Liewig, Jamhuri Kihwelo, Dk. Cosmas Kapinga, James Kisaka na Kessy Rajab.
 
Simba inaondoka kwa ndege ya Shirika la Ndege la Kenya (Kenya Airways) majira ya saa 11:10 alfajiri na inatarajiwa kufika Luanda, Angola majira ya saa nne asubuhi.
 
Timu itafanya mazoezi ya mwisho jijini Dar es Salaam leo jioni kabla ya kuelekea kambini ambapo wachezaji watapumzika kusubiri muda wa safari.
 
Mechi kati ya Simba na Libolo itachezwa Machi 3 (Jumapili ijayo) katika Uwanja wa Calulo uliopo katika mji wa Calulo jimbo la Kwanza Sul (Kwanza Kusini).
 

Umeiona hii.

haya ndiyo yaliyotokea usiku huu baada ya kuchapwa Arsenal Goli mbili maisha jamaa half time tu alipatwa na usingizi wa kutosha na kutokea dirishani baada ya wapinza kufunga mlango na kumzuia kutoka. je wewe mshabiki sugu wa Arsenal ulihimiri.

MSIGWA CUP YAANZA NUSU FAINALI.



Michuano ya Msigwa Cup imeendelea hii leo kwa mchezo wa nusu fainali ya kwanza kati ya chuo cha maendeleo ya jamii CDTI na Polisi ya Iringa ambapo mchezo huo umemalizika kwa matokeo ya timu ya Polisi kushinda magoli 2 kwa 0.

NI KIBARUA PRISONS, SIMBA JIJINI MBEYA

BAADA ya sare mbili mfululizo, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL), Simba kesho (Februari 20 mwaka huu) wanashuka Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya wakiwa wageni wa Tanzania Prisons.

Katika mechi zake mbili zilizopita, Simba iliondoka pointi mbili tu kati ya sita ilizokuwa ikizipigania. Ilitoka sare na timu za JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na baadaye sare ya 1-1 ugenini dhidi ya Oljoro JKT.

Hiyo itakuwa mechi ya nne kwa Mfaransa Patrick Liewig tangu aanze kuinoa Simba huku akifanikiwa kuondoka na ushindi katika mechi moja dhidi ya African Lyon inayokamata mkia kwenye ligi hiyo. Simba iliilaza Lyon mabao 3-1.

Kwa upande wa kocha Jumanne Chale anashusha kikosi chake uwanjani kesho akiwa na kumbukumbu nzuri ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya African Lyon katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja huo huo Februari 9 mwaka huu.

Hekaheka nyingine itakuwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 25,000 utakapokuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto Africans na African Lyon. Wakati Lyon ikikamata mkia, Toto Africans yenye pointi 14 inashika nafasi ya 12 katika ligi hiyo inayoshirikisha timu 14.

Mwamuzi Simon Mberwa wa Pwani atakuwa shuhuda wa mechi kati ya Coastal Union ya Tanga na Oljoro JKT ya Arusha itakayofanyika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga. Mechi hiyo inatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na uimara wa timu zote mbili.

Nayo JKT Ruvu ambayo haijafanya vizuri msimu huu kulinganisha na minne iliyopita itacheza Azam kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam. JKT Ruvu chini ya kocha Charles Kilinda inakamata nafasi ya nne kutoka chini ikiwa na pointi 16 baada ya kucheza mechi 15.

Iwapo itafanikiwa kushinda mechi hiyo, Azam itaendelea kujiimarisha katika nafasi ya pili nyuma ya vinara Yanga. Azam ambayo ni moja ya timu zenye safu kali ya ushambuliaji katika ligi hiyo ikiwa imefunga mabao 27 ina pointi 33.

FIFA YASITISHA MCHAKATO WA UCHAGUZI TFF



SHIRIKISHO la Kimaifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limeahirisha uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kutokana na mkanganyiko uliojitokeza katika mchakato wa uchaguzi huo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari katika ofisi za TFF jijini Dar es Salaam leo mchana (Februari 19 mwaka huu), Rais wa TFF, Leodegar Tenga amesema FIFA imetuma barua ikiagiza mchakato wa uchaguzi usimame baada ya kupata malalamiko.

Amesema kutokana na mkanganyiko huo, FIFA katika barua yake ya leo (Februari 19 mwaka huu- imeambatanishwa) imeagiza mkutano wa uchaguzi wa TFF ambao awali ulipangwa kufanyika Februari 24 mwaka huu uahirishwe hadi hapo itakapotuma ujumbe wake nchini.

Ujumbe huo wa FIFA unatarajiwa kufika nchini katikati ya mwezi ujao (Machi) ambapo utafanya tathimini ya hali hivyo, kutuma ripoti yake katika shirikisho hilo na baadaye kutoa mwongozo wa nini kifanyike.

Rais Tenga amewaomba radhi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF kwa usumbufu uliojitokeza kutokana na uamuzi huo wa FIFA, hivyo kwa sasa hakutakuwa tena na mkutano huo mpaka hapo watakapopewa taarifa nyingi.

Amesema TFF inakaribisha kwa mikono miwili uamuzi huo wa FIFA kwa sababu ni chombo ambacho cha juu kimpira duniani, na hatua hiyo ina lengo la kuhakikisha kuwa kila mhusika katika mchakato huo wa uchaguzi anapata haki yake.

“Nia yetu ni kuona watu wanatendewa haki, na nia ya FIFA ni kutafuta ukweli. Hivyo wahusika (waathirika) wajiandae, watumie wakati huu kuandaa hoja zao ili FIFA wakifika wawasikilize, wapate maelezo ya kina kuhusu utaratibu na malalamiko yaliyotolewa,” alisema Tenga.

Rais Tenga amesema timu hiyo ya FIFA itakapofika yenyewe ndiyo itakayopanga izungumze na nani kwa wakati gani, hivyo ni vizuri waathirika na vyombo vyote vilivyohusika na mchakato wa uchaguzi wakajiandaa.

Amesema ilikuwa ni muhimu suala hili likatatuliwa katika ngazi ya FIFA kwa lengo la kuhakikisha uchaguzi utakapofanyika TFF inaendelea kuwa chombo kimoja badala ya kurudi katika migogoro iliyokuwepo huko nyuma.

“Nataka tubakie kama tulivyokuwa. Malumbano yaishe. Pangeni hoja, wakija hao waheshimiwa (FIFA) muwaambie. FIFA ni chombo cha juu, nafurahi wamekubali kuingia katika hili, kwani wana shughuli nyingi wangeweza kukataa,” amesema.

Kuhusu fursa ya kufanya marejeo (review) kwenye Kamati ya Rufani ya Uchaguzi inayoongozwa na Idd Mtiginjola ambayo aliielezea Jumamosi, Rais Tenga amesema kwa vile hicho ndicho chombo cha mwisho nchini katika masuala ya uchaguzi alishauriwa kuwa kingeweza kufanya review.

“Kwa vile hakuna chombo kingine, nikashauriwa kuwa kinaweza kufanya review. Katika utaratibu wa kutoa haki, uamuzi ni lazima uwe wa wazi kwa kutoa sababu. Nilidhani hilo linawezekana, kwani Mahakama Kuu hufanya hivyo. Kwa hili uamuzi wa Mtiginjola ni sahihi,” amesema Rais Tenga.

Kamati ya Mtiginjola iliyokutana jana (Februari 18 mwaka huu) ilitupa maombi ya review yaliyowasilishwa mbele yake na waombaji uongozi watano kwa vile hakuna kipengele chochote kwenye Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi kinachotoa fursa hiyo.

Waombaji hao walikuwa Jamal Emil Malinzi aliyeenguliwa kugombea urais wa TFF na Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye kinyang’anyiro cha kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).

Wengine ni walioomba kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF na Kanda zao kwenye mabano; Eliud Peter Mvella (Iringa na Mbeya), Farid Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu).

HABAI HIZI NAZO ZILIKUWEMO

SIMBA YAINGIZA MIL 134/-, AZAM MIL 34/-
PAMBANO la Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Simba na Libolo FC ya Angola lililofanyika jana (Februari 17 mwaka huu) limeingiza sh. 133,795,000 wakati lile la Kombe la Shirikisho kati ya Azam na El Nasir ya Sudan Kusini lililochezwa juzi (Februari 16 mwaka huu) limeingiza sh. 34,046,000.

Watazamaji 22,469 walikata tiketi kushuhudia mechi ya Simba kwa viingilio vya sh. 5,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000. Simba ilipoteza pambano hilo kwa bao 1-0.

Mgawo wa mechi hiyo ulikuwa kama ifuatavyo; gharama za waamuzi sh. 24,926,500, gharama za tiketi sh. 7,410,000, asilimia 15 ya uwanja baada ya kuondoa gharama za waamuzi na tiketi ilikuwa sh. 15,218,775, asilimia 10 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 10,145,850 na asilimia 75 iliyokwenda klabu ya Simba ni sh. 76,093,875.

Mechi ya Azam iliyomalizika kwa wenyeji kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 ilishuhudiwa na watazamaji 13,431 kwa viingilio vya sh. 2,000, sh. 5,000, sh. 10,000 na sh. 20,000. Mgawo katika mechi hiyo ulikuwa kama ifuatavyo;

Gharama za tiketi sh. 4,779,000, asilimia 15 ya uwanja baada ya kuondoa gharama za tiketi ilikuwa sh. 4,390,050, asilimia 10 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 2,926,700 na asilimia 75 iliyokwenda Prime Time Promotions (Azam) ni sh. 29,267,00.

PONGEZI KWA UONGOZI MPYA SPUTANZA, FRAT
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa uongozi mpya wa Chama cha Wachezaji Mpira wa Miguu Tanzania (SPUTANZA) na wa Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) uliochaguliwa wiki iliyopita.

Uongozi wa FRAT ulichaguliwa Februari 13 mwaka huu mjini Morogoro wakati wa SPUTANZA ulichaguliwa jana (Februari 17 mwaka huu) katika uchaguzi uliofanyika Kigamboni, Dar es Salaam.

Waliochaguliwa kuongoza SPUTANZA na hawakuwa na wapinzani ni Musa Kissoky (Mwenyekiti) na Said George (Katibu Mkuu) wakati Ali Mayai aliwashinda Isaac Mwakatika na Hakim Byemba katika nafasi ya mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF.

Kusianga Kiata na Charles Mngodo walichaguliwa kuwa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya SPUTANZA. Katika uchaguzi huo uliohudhuriwa na wapiga kura 17, Mhazini na nafasi moja ya mjumbe wa Kamati ya Utendaji zitajazwa baadaye kutokana na kukosa wagombea.

Kwa upande wa FRAT viongozi waliochaguliwa ni Said Nassoro (Mwenyekiti), Charles Ndagala (Katibu Mkuu) na Kamwanga Tambwe (mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF).

Ushindi waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza vyama hivyo unaonesha jinsi wapiga kura walivyo na imani kubwa kwao, na TFF inaahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya FRAT na SPUTANZA.

Uongozi huo mpya una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni kuhakikisha unaendesha shughuli za mpira wa miguu kwa kuzingatia katiba zao pamoja na vyombo vya mpira wa miguu vilivyo juu yao.

Pia tunatoa pongezi kwa kamati za uchaguzi za FRAT na SPUTANZA na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa kuhakikisha uchaguzi umeendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za

Kamati ya Mtnginjola yaendeleza kiburi




KAMATI ya Rufani ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inayoongozwa na Idd Mtiginjola imetupa maombi ya kufanyia marejeo (review) uamuzi wake kama yalivyowasilishwa mbele yake na waombaji watano.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za TFF, Dar es Salaam leo mchana (Februari 18 mwaka huu), Mtiginjola ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo amesema wamepitia Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi za TFF na kubaini kuwa hakuna Ibara yoyote inayotoa fursa ya review kwa uamuzi ambao wameshaufanya.

Amesema Kanuni za Mwenendo wa Madai (CPC) katika mahakama za kawaida zinaruhusu Hakimu aliyefanya uamuzi katika kesi kufanya marejeo, lakini katika masuala ya mpira wa miguu hakuna fursa hiyo, hivyo hawawezi kujitungia kitu kipya kwani kazi yao ni kufanya uamuzi kwa kutafsiri Katiba na kanuni walizopewa na mamlaka ya uteuzi (TFF).

Waombaji watano waliokuwa wakitaka Kamati hiyo ifanyie marejeo uamuzi wake kutupa rufani zao ni Jamal Emil Malinzi aliyeenguliwa kugombea urais wa TFF na Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye kinyang’anyiro cha kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).

Wengine ambao waliomba kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF na Kanda zao kwenye mabano ni Eliud Peter Mvella (Iringa na Mbeya), Farid Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu).