
Michuano ya
Msigwa Cup imeendelea hii leo kwa mchezo wa nusu fainali ya kwanza kati ya chuo
cha maendeleo ya jamii CDTI na Polisi ya Iringa ambapo mchezo huo umemalizika
kwa matokeo ya timu ya Polisi kushinda magoli 2 kwa 0.
BAADA
ya sare mbili mfululizo, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom
(VPL), Simba kesho (Februari 20 mwaka huu) wanashuka Uwanja wa
Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya wakiwa wageni wa Tanzania Prisons.
Katika
mechi zake mbili zilizopita, Simba iliondoka pointi mbili tu kati ya
sita ilizokuwa ikizipigania. Ilitoka sare na timu za JKT Ruvu kwenye
Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na baadaye sare ya 1-1 ugenini dhidi ya
Oljoro JKT.
Hiyo
itakuwa mechi ya nne kwa Mfaransa Patrick Liewig tangu aanze kuinoa
Simba huku akifanikiwa kuondoka na ushindi katika mechi moja dhidi ya
African Lyon inayokamata mkia kwenye ligi hiyo. Simba iliilaza Lyon
mabao 3-1.
Kwa
upande wa kocha Jumanne Chale anashusha kikosi chake uwanjani kesho
akiwa na kumbukumbu nzuri ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya
African Lyon katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja huo huo Februari 9
mwaka huu.
Hekaheka
nyingine itakuwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wenye uwezo wa
kuchukua watazamaji 25,000 utakapokuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto
Africans na African Lyon. Wakati Lyon ikikamata mkia, Toto Africans
yenye pointi 14 inashika nafasi ya 12 katika ligi hiyo inayoshirikisha
timu 14.
Mwamuzi
Simon Mberwa wa Pwani atakuwa shuhuda wa mechi kati ya Coastal Union ya
Tanga na Oljoro JKT ya Arusha itakayofanyika Uwanja wa Mkwakwani jijini
Tanga. Mechi hiyo inatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na
uimara wa timu zote mbili.
Nayo
JKT Ruvu ambayo haijafanya vizuri msimu huu kulinganisha na minne
iliyopita itacheza Azam kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es
Salaam. JKT Ruvu chini ya kocha Charles Kilinda inakamata nafasi ya nne
kutoka chini ikiwa na pointi 16 baada ya kucheza mechi 15.
Iwapo
itafanikiwa kushinda mechi hiyo, Azam itaendelea kujiimarisha katika
nafasi ya pili nyuma ya vinara Yanga. Azam ambayo ni moja ya timu zenye
safu kali ya ushambuliaji katika ligi hiyo ikiwa imefunga mabao 27 ina
pointi 33.
SHIRIKISHO la Kimaifa la Mpira wa
Miguu (FIFA) limeahirisha uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania
(TFF) kutokana na mkanganyiko uliojitokeza katika mchakato wa uchaguzi huo.
Akizungumza na Waandishi wa
Habari katika ofisi za TFF jijini Dar es Salaam leo mchana (Februari 19 mwaka
huu), Rais wa TFF, Leodegar Tenga amesema FIFA imetuma barua ikiagiza mchakato
wa uchaguzi usimame baada ya kupata malalamiko.
Amesema kutokana na mkanganyiko
huo, FIFA katika barua yake ya leo (Februari 19 mwaka huu- imeambatanishwa)
imeagiza mkutano wa uchaguzi wa TFF ambao awali ulipangwa kufanyika Februari 24
mwaka huu uahirishwe hadi hapo itakapotuma ujumbe wake nchini.
Ujumbe huo wa FIFA unatarajiwa
kufika nchini katikati ya mwezi ujao (Machi) ambapo utafanya tathimini ya hali
hivyo, kutuma ripoti yake katika shirikisho hilo na baadaye kutoa mwongozo wa
nini kifanyike.
Rais Tenga amewaomba radhi
wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF kwa usumbufu uliojitokeza kutokana na uamuzi huo
wa FIFA, hivyo kwa sasa hakutakuwa tena na mkutano huo mpaka hapo watakapopewa
taarifa nyingi.
Amesema TFF inakaribisha kwa
mikono miwili uamuzi huo wa FIFA kwa sababu ni chombo ambacho cha juu kimpira
duniani, na hatua hiyo ina lengo la kuhakikisha kuwa kila mhusika katika
mchakato huo wa uchaguzi anapata haki yake.
“Nia yetu ni kuona watu
wanatendewa haki, na nia ya FIFA ni kutafuta ukweli. Hivyo wahusika
(waathirika) wajiandae, watumie wakati huu kuandaa hoja zao ili FIFA wakifika
wawasikilize, wapate maelezo ya kina kuhusu utaratibu na malalamiko
yaliyotolewa,” alisema Tenga.
Rais Tenga amesema timu hiyo ya
FIFA itakapofika yenyewe ndiyo itakayopanga izungumze na nani kwa wakati gani,
hivyo ni vizuri waathirika na vyombo vyote vilivyohusika na mchakato wa
uchaguzi wakajiandaa.
Amesema ilikuwa ni muhimu suala
hili likatatuliwa katika ngazi ya FIFA kwa lengo la kuhakikisha uchaguzi
utakapofanyika TFF inaendelea kuwa chombo kimoja badala ya kurudi katika
migogoro iliyokuwepo huko nyuma.
“Nataka tubakie kama tulivyokuwa.
Malumbano yaishe. Pangeni hoja, wakija hao waheshimiwa (FIFA) muwaambie. FIFA
ni chombo cha juu, nafurahi wamekubali kuingia katika hili, kwani wana shughuli
nyingi wangeweza kukataa,” amesema.
Kuhusu fursa ya kufanya marejeo
(review) kwenye Kamati ya Rufani ya Uchaguzi inayoongozwa na Idd Mtiginjola
ambayo aliielezea Jumamosi, Rais Tenga amesema kwa vile hicho ndicho chombo cha
mwisho nchini katika masuala ya uchaguzi alishauriwa kuwa kingeweza kufanya
review.
“Kwa vile hakuna chombo kingine,
nikashauriwa kuwa kinaweza kufanya review. Katika utaratibu wa kutoa haki,
uamuzi ni lazima uwe wa wazi kwa kutoa sababu. Nilidhani hilo linawezekana,
kwani Mahakama Kuu hufanya hivyo. Kwa hili uamuzi wa Mtiginjola ni sahihi,”
amesema Rais Tenga.
Kamati ya Mtiginjola iliyokutana
jana (Februari 18 mwaka huu) ilitupa maombi ya review yaliyowasilishwa mbele
yake na waombaji uongozi watano kwa vile hakuna kipengele chochote kwenye
Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi kinachotoa fursa hiyo.
Waombaji hao walikuwa Jamal Emil
Malinzi aliyeenguliwa kugombea urais wa TFF na Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye
kinyang’anyiro cha kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).
Wengine ni walioomba kuwania
ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF na Kanda zao kwenye mabano; Eliud Peter
Mvella (Iringa na Mbeya), Farid Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha
Matutu (Shinyanga na Simiyu).
SIMBA YAINGIZA MIL 134/-, AZAM MIL 34/-
PAMBANO
la Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Simba na Libolo FC ya Angola
lililofanyika jana (Februari 17 mwaka huu) limeingiza sh. 133,795,000
wakati lile la Kombe la Shirikisho kati ya Azam na El Nasir ya Sudan
Kusini lililochezwa juzi (Februari 16 mwaka huu) limeingiza sh.
34,046,000.
Watazamaji
22,469 walikata tiketi kushuhudia mechi ya Simba kwa viingilio vya sh.
5,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000. Simba ilipoteza
pambano hilo kwa bao 1-0.
Mgawo
wa mechi hiyo ulikuwa kama ifuatavyo; gharama za waamuzi sh.
24,926,500, gharama za tiketi sh. 7,410,000, asilimia 15 ya uwanja baada
ya kuondoa gharama za waamuzi na tiketi ilikuwa sh. 15,218,775,
asilimia 10 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Shirikisho
la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 10,145,850 na asilimia 75
iliyokwenda klabu ya Simba ni sh. 76,093,875.
Mechi
ya Azam iliyomalizika kwa wenyeji kuibuka na ushindi wa mabao 3-1
ilishuhudiwa na watazamaji 13,431 kwa viingilio vya sh. 2,000, sh.
5,000, sh. 10,000 na sh. 20,000. Mgawo katika mechi hiyo ulikuwa kama
ifuatavyo;
Gharama
za tiketi sh. 4,779,000, asilimia 15 ya uwanja baada ya kuondoa gharama
za tiketi ilikuwa sh. 4,390,050, asilimia 10 ya Shirikisho la Mpira wa
Miguu Tanzania (TFF) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh.
2,926,700 na asilimia 75 iliyokwenda Prime Time Promotions (Azam) ni sh.
29,267,00.
PONGEZI KWA UONGOZI MPYA SPUTANZA, FRAT
Shirikisho
la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa uongozi mpya wa
Chama cha Wachezaji Mpira wa Miguu Tanzania (SPUTANZA) na wa Chama cha
Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) uliochaguliwa wiki iliyopita.
Uongozi
wa FRAT ulichaguliwa Februari 13 mwaka huu mjini Morogoro wakati wa
SPUTANZA ulichaguliwa jana (Februari 17 mwaka huu) katika uchaguzi
uliofanyika Kigamboni, Dar es Salaam.
Waliochaguliwa
kuongoza SPUTANZA na hawakuwa na wapinzani ni Musa Kissoky (Mwenyekiti)
na Said George (Katibu Mkuu) wakati Ali Mayai aliwashinda Isaac
Mwakatika na Hakim Byemba katika nafasi ya mjumbe wa Mkutano Mkuu wa
TFF.
Kusianga
Kiata na Charles Mngodo walichaguliwa kuwa wajumbe wa Kamati ya
Utendaji ya SPUTANZA. Katika uchaguzi huo uliohudhuriwa na wapiga kura
17, Mhazini na nafasi moja ya mjumbe wa Kamati ya Utendaji zitajazwa
baadaye kutokana na kukosa wagombea.
Kwa
upande wa FRAT viongozi waliochaguliwa ni Said Nassoro (Mwenyekiti),
Charles Ndagala (Katibu Mkuu) na Kamwanga Tambwe (mjumbe wa Mkutano Mkuu
wa TFF).
Ushindi
waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza vyama hivyo unaonesha jinsi
wapiga kura walivyo na imani kubwa kwao, na TFF inaahidi kuendeleza
ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya FRAT na SPUTANZA.
Uongozi
huo mpya una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni kuhakikisha unaendesha
shughuli za mpira wa miguu kwa kuzingatia katiba zao pamoja na vyombo
vya mpira wa miguu vilivyo juu yao.
KAMATI ya Rufani ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa
Miguu Tanzania (TFF) inayoongozwa na Idd Mtiginjola imetupa maombi ya kufanyia
marejeo (review) uamuzi wake kama yalivyowasilishwa mbele yake na waombaji
watano.
Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za
TFF, Dar es Salaam leo mchana (Februari 18 mwaka huu), Mtiginjola ambaye ni
Mwenyekiti wa Kamati hiyo amesema wamepitia Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi
za TFF na kubaini kuwa hakuna Ibara yoyote inayotoa fursa ya review kwa uamuzi
ambao wameshaufanya.
Amesema Kanuni za Mwenendo wa Madai (CPC) katika
mahakama za kawaida zinaruhusu Hakimu aliyefanya uamuzi katika kesi kufanya
marejeo, lakini katika masuala ya mpira wa miguu hakuna fursa hiyo, hivyo
hawawezi kujitungia kitu kipya kwani kazi yao ni kufanya uamuzi kwa kutafsiri
Katiba na kanuni walizopewa na mamlaka ya uteuzi (TFF).
Waombaji watano waliokuwa wakitaka Kamati hiyo ifanyie
marejeo uamuzi wake kutupa rufani zao ni Jamal Emil Malinzi aliyeenguliwa
kugombea urais wa TFF na Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye kinyang’anyiro cha
kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).
Wengine ambao waliomba kuwania ujumbe wa Kamati ya
Utendaji ya TFF na Kanda zao kwenye mabano ni Eliud Peter Mvella (Iringa na
Mbeya), Farid Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha Matutu (Shinyanga na
Simiyu).
Rais
wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga
amewataka waombaji uongozi ambao hawaridhiki na uamuzi wa Kamati ya
Rufani ya Uchaguzi kutafuta haki yao kwa mujibu wa taratibu zilizopo.
Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam leo (Februari 16 mwaka huu) mchana, Rais Tenga amesema TFF ni moja ya taasisi ambazo zina utaratibu unaoeleweka kwa wadau wake.
“Wote
tunafahamu taratibu ambazo tumejiwekea juu ya wagombea wetu
wanachaguliwaje. TFF ni moja ya taasisi ambazo zina utaratibu
unaoeleweka. Hii ni kuanzia wilayani. Kama kuna tatizo zipo njia za
kufuata.
“Katika
mchakato wa uchaguzi wengine wanafanikiwa, wengine wanaachwa. Wameachwa
kwa sababu zilizotolewa na Kamati ya Rufani ya Uchaguzi. Ambaye
haridhiki anafuata taratibu tulizojiwekea. Atafute haki yake kwa mujibu
wa taratibu,” amesema.
Rais
Tenga amesisitiza kuwa kikatiba hana uwezo wa kuingilia uamuzi
unaofanywa na kamati ambazo ameziunda, kwani utawala bora ni kusimamia
kanuni ambapo wanaofanya uamuzi lazima waweke wazi sababu za uamuzi
waliofikia.
Amesema
ambao hawakubaliani na uamuzi wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF
dhidi yao wana njia tatu za kufuata. Njia hizo ni kuiomba Kamati ya
Rufani ya Uchaguzi ipitie uamuzi iliofanya (review), kuandika Shirikisho
la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kuomba liingilie au kwenda
Mahakama ya Usuluhishi ya Michezo (CAS).
“Hata
ukiweka ngazi nne, mtu akiathirika ataona ameonewa tu. Kwa Katiba yetu
hapa (Kamati ya Rufani ya Uchaguzi) ndiyo mwisho. Hakuna chombo kingine.
Ukiwaomba FIFA waingilie, watakuja na tutawaeleza mchakato wote
ulivyokwenda. Tunapenda kuwahakikishia hawa (waathirika) kuwa kwa
maslahi ya mpira wa miguu tutasaidia katika hilo wapate haki,” amesema
Rais Tenga na kuongeza kuwa tayari waathirika wawili wa uamuzi wa Kamati
ya Rufani ya Uchaguzi wameomba marejeo (review) kwenye kamati hiyo
hiyo.
Amesema
TFF imelazimika kuzungumzia suala hilo kwa sababu limekuwa
likizungumzwa kinazi zaidi wakati taratibu ziko wazi, hivyo kwa maslahi
ya mpira wa miguu ni vizuri taratibu zikafuatwa.
“Nawaomba
washabiki wa mpira wa miguu, tumejenga chombo hiki (TFF) kwa muda
mrefu. Bado tunaomba watu watusaidie, kwa hiyo matusi hayawezi kubadili
kitu. Tunachowahakikishia ni kuwa, mtu anapoomba msaada tutampa kutafuta
haki yake.
“Hizi
ni kamati huru, lazima ziheshimiwe. Ukianza kuziingilia utakuwa umeua
mpira wa miguu. Uongozi ni utumishi, tusionekane tunagombana. Huu si
ubunge, mbunge anachaguliwa anakwenda kulipwa mshahara. Mjumbe wa Kamati
ya Utendaji ya TFF halipwi mshahara. Tusirudi kwenye matusi,
tulishaondoka huko,” amesema.
Kuhusu
mabadiliko ya Katiba yaliyofanyika kwa njia ya waraka, Rais Tenga
amesema yamefanyika kwa mujibu wa taratibu, na haikuwa siri. Maeneo
yaliyofanyiwa marekebisho ilikuwa ni lazima, kwani mengi yalikuwa ni
maagizo kutoka FIFA na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).
Amesisitiza
kuwa mabadiliko hayo yamefuata taratibu na hakuna udanganyifu katika
hilo, kwani ridhaa ya kutumia waraka iliombwa, na Mkutano ni watu ambao
ndiyo wamepitisha mabadiliko hayo.
“Mkutano
Mkuu ni watu, si kikao. Katika dunia ya leo mikutano inafanyika kwa
tele conference, si lazima watu wakutane sehemu moja,” amesema na
kuongeza kuwa mabadiliko hayo yalipitishwa kwa kura 70 dhidi ya 33
zilizokataa.
Kuhusu
Kanuni kusainiwa kabla ya Katiba, Rais Tenga amesema tarehe ya kuanza
kutumika Katiba ni siku ridhaa ilipopatikana, na si siku mhuri wa
Msajili ulipopigwa. Mabadiliko ya Katiba yalipita Desemba 15 mwaka jana,
Kanuni zilisainiwa Januari 7 mwaka huu.
Uchaguzi wa TFF umesitishwa katika tarehe iliyopangwa kwa mujibu wa Ibara ya 10(5) Tff imesitisha uchaguzi huo kutokana na mamlaka yake hadi hapo itakapo maliza matatizo ya kikatiba.
taarifa hiyo imeetolewa leo na mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi Deogratius Lyato.
Chaguzi za TFF kwa upande wa TBL BOARD ulitakiwa kufanyika February 22 na TFF February 24.
Subscribe to:
Posts (Atom)