Umeiona hii.

haya ndiyo yaliyotokea usiku huu baada ya kuchapwa Arsenal Goli mbili maisha jamaa half time tu alipatwa na usingizi wa kutosha na kutokea dirishani baada ya wapinza kufunga mlango na kumzuia kutoka. je wewe mshabiki sugu wa Arsenal ulihimiri.

MSIGWA CUP YAANZA NUSU FAINALI.



Michuano ya Msigwa Cup imeendelea hii leo kwa mchezo wa nusu fainali ya kwanza kati ya chuo cha maendeleo ya jamii CDTI na Polisi ya Iringa ambapo mchezo huo umemalizika kwa matokeo ya timu ya Polisi kushinda magoli 2 kwa 0.

NI KIBARUA PRISONS, SIMBA JIJINI MBEYA

BAADA ya sare mbili mfululizo, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL), Simba kesho (Februari 20 mwaka huu) wanashuka Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya wakiwa wageni wa Tanzania Prisons.

Katika mechi zake mbili zilizopita, Simba iliondoka pointi mbili tu kati ya sita ilizokuwa ikizipigania. Ilitoka sare na timu za JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na baadaye sare ya 1-1 ugenini dhidi ya Oljoro JKT.

Hiyo itakuwa mechi ya nne kwa Mfaransa Patrick Liewig tangu aanze kuinoa Simba huku akifanikiwa kuondoka na ushindi katika mechi moja dhidi ya African Lyon inayokamata mkia kwenye ligi hiyo. Simba iliilaza Lyon mabao 3-1.

Kwa upande wa kocha Jumanne Chale anashusha kikosi chake uwanjani kesho akiwa na kumbukumbu nzuri ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya African Lyon katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja huo huo Februari 9 mwaka huu.

Hekaheka nyingine itakuwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 25,000 utakapokuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto Africans na African Lyon. Wakati Lyon ikikamata mkia, Toto Africans yenye pointi 14 inashika nafasi ya 12 katika ligi hiyo inayoshirikisha timu 14.

Mwamuzi Simon Mberwa wa Pwani atakuwa shuhuda wa mechi kati ya Coastal Union ya Tanga na Oljoro JKT ya Arusha itakayofanyika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga. Mechi hiyo inatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na uimara wa timu zote mbili.

Nayo JKT Ruvu ambayo haijafanya vizuri msimu huu kulinganisha na minne iliyopita itacheza Azam kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam. JKT Ruvu chini ya kocha Charles Kilinda inakamata nafasi ya nne kutoka chini ikiwa na pointi 16 baada ya kucheza mechi 15.

Iwapo itafanikiwa kushinda mechi hiyo, Azam itaendelea kujiimarisha katika nafasi ya pili nyuma ya vinara Yanga. Azam ambayo ni moja ya timu zenye safu kali ya ushambuliaji katika ligi hiyo ikiwa imefunga mabao 27 ina pointi 33.

FIFA YASITISHA MCHAKATO WA UCHAGUZI TFF



SHIRIKISHO la Kimaifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limeahirisha uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kutokana na mkanganyiko uliojitokeza katika mchakato wa uchaguzi huo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari katika ofisi za TFF jijini Dar es Salaam leo mchana (Februari 19 mwaka huu), Rais wa TFF, Leodegar Tenga amesema FIFA imetuma barua ikiagiza mchakato wa uchaguzi usimame baada ya kupata malalamiko.

Amesema kutokana na mkanganyiko huo, FIFA katika barua yake ya leo (Februari 19 mwaka huu- imeambatanishwa) imeagiza mkutano wa uchaguzi wa TFF ambao awali ulipangwa kufanyika Februari 24 mwaka huu uahirishwe hadi hapo itakapotuma ujumbe wake nchini.

Ujumbe huo wa FIFA unatarajiwa kufika nchini katikati ya mwezi ujao (Machi) ambapo utafanya tathimini ya hali hivyo, kutuma ripoti yake katika shirikisho hilo na baadaye kutoa mwongozo wa nini kifanyike.

Rais Tenga amewaomba radhi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF kwa usumbufu uliojitokeza kutokana na uamuzi huo wa FIFA, hivyo kwa sasa hakutakuwa tena na mkutano huo mpaka hapo watakapopewa taarifa nyingi.

Amesema TFF inakaribisha kwa mikono miwili uamuzi huo wa FIFA kwa sababu ni chombo ambacho cha juu kimpira duniani, na hatua hiyo ina lengo la kuhakikisha kuwa kila mhusika katika mchakato huo wa uchaguzi anapata haki yake.

“Nia yetu ni kuona watu wanatendewa haki, na nia ya FIFA ni kutafuta ukweli. Hivyo wahusika (waathirika) wajiandae, watumie wakati huu kuandaa hoja zao ili FIFA wakifika wawasikilize, wapate maelezo ya kina kuhusu utaratibu na malalamiko yaliyotolewa,” alisema Tenga.

Rais Tenga amesema timu hiyo ya FIFA itakapofika yenyewe ndiyo itakayopanga izungumze na nani kwa wakati gani, hivyo ni vizuri waathirika na vyombo vyote vilivyohusika na mchakato wa uchaguzi wakajiandaa.

Amesema ilikuwa ni muhimu suala hili likatatuliwa katika ngazi ya FIFA kwa lengo la kuhakikisha uchaguzi utakapofanyika TFF inaendelea kuwa chombo kimoja badala ya kurudi katika migogoro iliyokuwepo huko nyuma.

“Nataka tubakie kama tulivyokuwa. Malumbano yaishe. Pangeni hoja, wakija hao waheshimiwa (FIFA) muwaambie. FIFA ni chombo cha juu, nafurahi wamekubali kuingia katika hili, kwani wana shughuli nyingi wangeweza kukataa,” amesema.

Kuhusu fursa ya kufanya marejeo (review) kwenye Kamati ya Rufani ya Uchaguzi inayoongozwa na Idd Mtiginjola ambayo aliielezea Jumamosi, Rais Tenga amesema kwa vile hicho ndicho chombo cha mwisho nchini katika masuala ya uchaguzi alishauriwa kuwa kingeweza kufanya review.

“Kwa vile hakuna chombo kingine, nikashauriwa kuwa kinaweza kufanya review. Katika utaratibu wa kutoa haki, uamuzi ni lazima uwe wa wazi kwa kutoa sababu. Nilidhani hilo linawezekana, kwani Mahakama Kuu hufanya hivyo. Kwa hili uamuzi wa Mtiginjola ni sahihi,” amesema Rais Tenga.

Kamati ya Mtiginjola iliyokutana jana (Februari 18 mwaka huu) ilitupa maombi ya review yaliyowasilishwa mbele yake na waombaji uongozi watano kwa vile hakuna kipengele chochote kwenye Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi kinachotoa fursa hiyo.

Waombaji hao walikuwa Jamal Emil Malinzi aliyeenguliwa kugombea urais wa TFF na Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye kinyang’anyiro cha kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).

Wengine ni walioomba kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF na Kanda zao kwenye mabano; Eliud Peter Mvella (Iringa na Mbeya), Farid Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu).

HABAI HIZI NAZO ZILIKUWEMO

SIMBA YAINGIZA MIL 134/-, AZAM MIL 34/-
PAMBANO la Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Simba na Libolo FC ya Angola lililofanyika jana (Februari 17 mwaka huu) limeingiza sh. 133,795,000 wakati lile la Kombe la Shirikisho kati ya Azam na El Nasir ya Sudan Kusini lililochezwa juzi (Februari 16 mwaka huu) limeingiza sh. 34,046,000.

Watazamaji 22,469 walikata tiketi kushuhudia mechi ya Simba kwa viingilio vya sh. 5,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000. Simba ilipoteza pambano hilo kwa bao 1-0.

Mgawo wa mechi hiyo ulikuwa kama ifuatavyo; gharama za waamuzi sh. 24,926,500, gharama za tiketi sh. 7,410,000, asilimia 15 ya uwanja baada ya kuondoa gharama za waamuzi na tiketi ilikuwa sh. 15,218,775, asilimia 10 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 10,145,850 na asilimia 75 iliyokwenda klabu ya Simba ni sh. 76,093,875.

Mechi ya Azam iliyomalizika kwa wenyeji kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 ilishuhudiwa na watazamaji 13,431 kwa viingilio vya sh. 2,000, sh. 5,000, sh. 10,000 na sh. 20,000. Mgawo katika mechi hiyo ulikuwa kama ifuatavyo;

Gharama za tiketi sh. 4,779,000, asilimia 15 ya uwanja baada ya kuondoa gharama za tiketi ilikuwa sh. 4,390,050, asilimia 10 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 2,926,700 na asilimia 75 iliyokwenda Prime Time Promotions (Azam) ni sh. 29,267,00.

PONGEZI KWA UONGOZI MPYA SPUTANZA, FRAT
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa uongozi mpya wa Chama cha Wachezaji Mpira wa Miguu Tanzania (SPUTANZA) na wa Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) uliochaguliwa wiki iliyopita.

Uongozi wa FRAT ulichaguliwa Februari 13 mwaka huu mjini Morogoro wakati wa SPUTANZA ulichaguliwa jana (Februari 17 mwaka huu) katika uchaguzi uliofanyika Kigamboni, Dar es Salaam.

Waliochaguliwa kuongoza SPUTANZA na hawakuwa na wapinzani ni Musa Kissoky (Mwenyekiti) na Said George (Katibu Mkuu) wakati Ali Mayai aliwashinda Isaac Mwakatika na Hakim Byemba katika nafasi ya mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF.

Kusianga Kiata na Charles Mngodo walichaguliwa kuwa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya SPUTANZA. Katika uchaguzi huo uliohudhuriwa na wapiga kura 17, Mhazini na nafasi moja ya mjumbe wa Kamati ya Utendaji zitajazwa baadaye kutokana na kukosa wagombea.

Kwa upande wa FRAT viongozi waliochaguliwa ni Said Nassoro (Mwenyekiti), Charles Ndagala (Katibu Mkuu) na Kamwanga Tambwe (mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF).

Ushindi waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza vyama hivyo unaonesha jinsi wapiga kura walivyo na imani kubwa kwao, na TFF inaahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya FRAT na SPUTANZA.

Uongozi huo mpya una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni kuhakikisha unaendesha shughuli za mpira wa miguu kwa kuzingatia katiba zao pamoja na vyombo vya mpira wa miguu vilivyo juu yao.

Pia tunatoa pongezi kwa kamati za uchaguzi za FRAT na SPUTANZA na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa kuhakikisha uchaguzi umeendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za

Kamati ya Mtnginjola yaendeleza kiburi




KAMATI ya Rufani ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inayoongozwa na Idd Mtiginjola imetupa maombi ya kufanyia marejeo (review) uamuzi wake kama yalivyowasilishwa mbele yake na waombaji watano.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za TFF, Dar es Salaam leo mchana (Februari 18 mwaka huu), Mtiginjola ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo amesema wamepitia Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi za TFF na kubaini kuwa hakuna Ibara yoyote inayotoa fursa ya review kwa uamuzi ambao wameshaufanya.

Amesema Kanuni za Mwenendo wa Madai (CPC) katika mahakama za kawaida zinaruhusu Hakimu aliyefanya uamuzi katika kesi kufanya marejeo, lakini katika masuala ya mpira wa miguu hakuna fursa hiyo, hivyo hawawezi kujitungia kitu kipya kwani kazi yao ni kufanya uamuzi kwa kutafsiri Katiba na kanuni walizopewa na mamlaka ya uteuzi (TFF).

Waombaji watano waliokuwa wakitaka Kamati hiyo ifanyie marejeo uamuzi wake kutupa rufani zao ni Jamal Emil Malinzi aliyeenguliwa kugombea urais wa TFF na Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye kinyang’anyiro cha kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).

Wengine ambao waliomba kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF na Kanda zao kwenye mabano ni Eliud Peter Mvella (Iringa na Mbeya), Farid Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu).

KAULI YA TENGA JUU YA UCHAGUZI.


Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amewataka waombaji uongozi ambao hawaridhiki na uamuzi wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi kutafuta haki yao kwa mujibu wa taratibu zilizopo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam leo (Februari 16 mwaka huu) mchana, Rais Tenga amesema  TFF ni moja ya taasisi ambazo zina utaratibu unaoeleweka kwa wadau wake.

“Wote tunafahamu taratibu ambazo tumejiwekea juu ya wagombea wetu wanachaguliwaje. TFF ni moja ya taasisi ambazo zina utaratibu unaoeleweka. Hii ni kuanzia wilayani. Kama kuna tatizo zipo njia za kufuata.

“Katika mchakato wa uchaguzi wengine wanafanikiwa, wengine wanaachwa. Wameachwa kwa sababu zilizotolewa na Kamati ya Rufani ya Uchaguzi. Ambaye haridhiki anafuata taratibu tulizojiwekea. Atafute haki yake kwa mujibu wa taratibu,” amesema.

Rais Tenga amesisitiza kuwa kikatiba hana uwezo wa kuingilia uamuzi unaofanywa na kamati ambazo ameziunda, kwani utawala bora ni kusimamia kanuni ambapo wanaofanya uamuzi lazima waweke wazi sababu za uamuzi waliofikia.

Amesema ambao hawakubaliani na uamuzi wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF dhidi yao wana njia tatu za kufuata. Njia hizo ni kuiomba Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ipitie uamuzi iliofanya (review), kuandika Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kuomba liingilie au kwenda Mahakama ya Usuluhishi ya Michezo (CAS).

“Hata ukiweka ngazi nne, mtu akiathirika ataona ameonewa tu. Kwa Katiba yetu hapa (Kamati ya Rufani ya Uchaguzi) ndiyo mwisho. Hakuna chombo kingine. Ukiwaomba FIFA waingilie, watakuja na tutawaeleza mchakato wote ulivyokwenda. Tunapenda kuwahakikishia hawa (waathirika) kuwa kwa maslahi ya mpira wa miguu tutasaidia katika hilo wapate haki,” amesema Rais Tenga na kuongeza kuwa tayari waathirika wawili wa uamuzi wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi wameomba marejeo (review) kwenye kamati hiyo hiyo.

Amesema TFF imelazimika kuzungumzia suala hilo kwa sababu limekuwa likizungumzwa kinazi zaidi wakati taratibu ziko wazi, hivyo kwa maslahi ya mpira wa miguu ni vizuri taratibu zikafuatwa.

“Nawaomba washabiki wa mpira wa miguu, tumejenga chombo hiki (TFF) kwa muda mrefu. Bado tunaomba watu watusaidie, kwa hiyo matusi hayawezi kubadili kitu. Tunachowahakikishia ni kuwa, mtu anapoomba msaada tutampa kutafuta haki yake.

“Hizi ni kamati huru, lazima ziheshimiwe. Ukianza kuziingilia utakuwa umeua mpira wa miguu. Uongozi ni utumishi, tusionekane tunagombana. Huu si ubunge, mbunge anachaguliwa anakwenda kulipwa mshahara. Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF halipwi mshahara. Tusirudi kwenye matusi, tulishaondoka huko,” amesema.

Kuhusu mabadiliko ya Katiba yaliyofanyika kwa njia ya waraka, Rais Tenga amesema yamefanyika kwa mujibu wa taratibu, na haikuwa siri. Maeneo yaliyofanyiwa marekebisho ilikuwa ni lazima, kwani mengi yalikuwa ni maagizo kutoka FIFA na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).

Amesisitiza kuwa mabadiliko hayo yamefuata taratibu na hakuna udanganyifu katika hilo, kwani ridhaa ya kutumia waraka iliombwa, na Mkutano ni watu ambao ndiyo wamepitisha mabadiliko hayo.

“Mkutano Mkuu ni watu, si kikao. Katika dunia ya leo mikutano inafanyika kwa tele conference, si lazima watu wakutane sehemu moja,” amesema na kuongeza kuwa mabadiliko hayo yalipitishwa kwa kura 70 dhidi ya 33 zilizokataa.

Kuhusu Kanuni kusainiwa kabla ya Katiba, Rais Tenga amesema tarehe ya kuanza kutumika Katiba ni siku ridhaa ilipopatikana, na si siku mhuri wa Msajili ulipopigwa. Mabadiliko ya Katiba yalipita Desemba 15 mwaka jana, Kanuni zilisainiwa Januari 7 mwaka huu.

UCHAGUZI TFF WAOTA MBAWA.

 
Uchaguzi wa TFF umesitishwa katika tarehe iliyopangwa kwa mujibu wa Ibara ya 10(5) Tff imesitisha uchaguzi huo kutokana na mamlaka yake hadi hapo itakapo maliza matatizo ya kikatiba.

taarifa hiyo imeetolewa  leo na mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi Deogratius Lyato.

Chaguzi za TFF kwa upande wa TBL BOARD ulitakiwa kufanyika February 22 na TFF February 24.